MUONGOZO MFUPI WA KILIMO BORA CHA MINAZI TANZANIA

MUONGOZO MFUPI WA KILIMO BORA CHA MINAZI.


Na Mr Mpinga +255 757 139 423
Kilimoforlife@gmail.com

MAZINGIRA YANAYOFAA KULIMA MINAZI

Sehemu zinazofaa kulima zao
la minazi lazima ziwe na mvua ya kutosha au ziwe na mabonde yenye unyevu ardhini.
Kiwango cha mvua kisichopunguwa milimita 1000 hadi 2000 kwa mwaka na
kiangazi kisichozidi miezi mitatu hadi minne.

Sehemu yenye joto la kutosha (23 hadi 30 nyuzi joto) na mwinuko kutoka usawa wa bahari usiozidi mita 600.
Minazi inapendelea mwangaza wajua, kwa hivyo isipandwe chini ya miti kama vile miembe au mikorosho.

UCHAGUZI WA ARDHI

Ni vyema kufanya uchaguzi wa ardhi inayofaa kwa minazi kabla ya kupanda.

ARDHI INAYOFAA KUPANDA MINAZI
Minazi inaweza kustawi katika aina nyingi za udongo, lakini hupendelea zaidi kichanga, tifutifu au kinongo.

Katika sehemu zinazoathiriwa na ukame minazi inaweza kupandwa kwenye maeneo ambayo kina cha maji ardhini wakati wa kiangazi hakizidi mita 3.5 kutoka usawa wa ardhi.

ARDHI ISIYOFAA KUPANDA MINAZI

Haifai kupanda minazi kwenye ardhi yenye mawe, miamba, jasi na maji yaliyotuama. Sehemu hizi hazifai kwa sababu mizizi ya minazi inapokutana na moja ya hivi, husababisha minazi kudumaa, kubadilika rangi ya makuti kuwa ya njano badala ya kijani, huacha kuzaa na minazi hatimaye hufa.
Vile vile ardhi yenye kutuamisha maji zaidi ya siku mbili haifai, kwani husababisha mizizi ya minazi kuoza, hivyo kushindwa kupata chakula ipasavyo na mara nyingi minazi kufa.

KUTAYARISHA SHAMBA

Baada ya kuchagua sehemu ambayo minazi itapandwa mkulima ni lazima atayarishe shamba mapema kabla ya mvua kuanza. Matayarisho hayo ni pamoja na kufyeka, kung'oa visiki na kuondoa takataka. Kufanya hivi hurahisisha kazi za badaaye hasa upimaji wa shamba, palizi na kuzuia wadudu kama vile chonga.

UPIMAJI WA SHAMBA

Upimaji wa shamba ni muhimu kabla ya kupanda miche ya minazi.
Mkulima anaweza kupima shamba lake kwa kuzingatia mambo yafuatayo:

(1) Iwapo mkulima anataka kuchanganya mazao mengine kwenye shamba la minazi kama vile michungwa, minanasi, mipera na migomba, inashauriwa kutumia mita 9 kati ya mnazi na mnazi. Mstari hadi mstari mita 15.

(2) Iwapo mkulima atapendelea kupanda minazi peke yake shambani inabidi atumie nafasi ya mita 9x9x9 pembe tatu. Nafasi ya aina hii inafaa kwenye sehemu zenye mvua ya kutosha kama Zanzibar, Tanga, Pangani, bonde la Ng'apa na Mikindani. Sehemu zenye mvua chache kama vile Mtwara, Lindi, Kisarawe, Kibaha na Morogoro inashauriwa kutumia nafasi ya mita 10 kutoka mnazi hadi mnazi na mita 10, kati ya mstari na mstari.

Upimaji wa Kilimo cha pembenne na pembe tatu

MICHE BORA KWA UPANDAJI

Kabla ya mkulima kupanda miche ya minazi hana budi kuchagua miche iliyo bora. Uwe haukushambuliwa na wadudu au magonjwa. Uwe na afya majani yake yawe kijani.
Uwe wenye majani yapatayo sita na uwe umekaa kitaluni kwa miezi 9 kama umenunuwa miche.

UCHIMBAJI WA MASHIMO NA UPANDAJI

Ni vizuri mashimo yachimbwe kabla ya mvua. Kipimo cha kila shimo ni sentimita 60 kwa urefu, upana na kina. Shimo linapochimbwa udongo wajuu utengwe mbali na udongo wa chini. Baadae changanya udongo wa juu na debe moja la samadi au mboji (compost) kama inapatikana. Weka udongo wajuu wenye rutuba zaidi kwanza kwenye shimo, halafu panda mche wako katika shimo. Rudishia udongo wa chini na kuhakikisha kuwa mche wako umeshindiliwa ili usimame barabara.


MBEGU BORA ZA TIKITI, VITUNGUU, NYANYA, HOHO, N.K 
UCHAGUZI WA MBEGU NA UPANDAJI.

UCHAGUZI WA MBEGU
Kilimo for life inashauri mkulima kuandaa mbegu ya nazi na kusia  moja kwa moja kuliko kutumia au kununuwa miche, hii ni kwa sababu ukinunua mche unakuwa hujui imetoka mnazi gani, wenye ubora gani na hata uzaaji wake huujui, lakini inashauriwa kununua nazi kutoka kwenye mnazi moja kwa moja kwa kuchagua mnazi bora na unaozaa nazi nyingi, Nzuri na kubwa, chagua nazi kubwa zaidi kutoka katika kila mnazi bora.

Nazi ambayo haijafuliwa inakuwa na pembe tatu, moja ya pembe hizi huwa kubwa zaidi na mbili zilizobaki hufanan ukubwa, ule upande mkubwa ulazwe chini wakati wa kupandwa, na upande ule wenye kikonyo ambako nazi hujishika katika matawi ya mnazi (mahanda) ndipo ambapo huota, utatakiwa upakate au upapunguze kwa kisu ili kurahisisha kuota, wakati wa kupanda hakikisha nazi ina maji, ikiwa na maji kidogo sana usiipande.

MUDA WA KUPANDA
panda miezi miwili au mitatu kabla ya mvua kuanza, nazi inauwezo wa kuota yenyewe bila mvua kwa sababu ina maji ndani yake, ila baada ya kuanza kuota kama hakuna mvua ni muhimu kumwagilia Laa sivyo mbegu yako itakufa.

KUMBUKA
Ni muhimu kuua mchwa shambani kwa kutumia Sumu au au oil chafu wakati wa kupanda, pia kuna baadhi ya mimea ambayo mizizi yake hufukuza mchwa inaweza kupandwa pamoja na nazi yako.

TAHADHARI Kama utaamua kutumia miche basi hakikisha miche yako haipungui umri wa miezi sita tangu mbegu kupandwa ili kuzuia miche mingi kufa.

ITAENDELEA.........

BONYEZAHAPA KUJIUNGA NA KUNDI LA KILIMO FOR LIFE FARMERS GROUP KWA MUONGOZO ZAIDI SHAMBANI 
MAWASILIANO
+255 757 139 423
Kilimoforlife@gmail.com
TEMBELEA
www.kilimoforlife.com

KWA MAKALA ZAIDI

Maoni

Machapisho Maarufu