kilimo bora cha tikiti maji

KILIMO CHA TIKITI MAJI TANZANIA




BONYEZA HAPA KUWASILIANA WHATSAPP

Habari mpenzi msomaji wa makala zetu za kilimo cha mazao mbalimbali kupitia mtandao wetu wa kilimo for life.
Leo tumeandaa makala maalumu juu ya kilimo cha kitaalamu na chenye faida zaidi cha tikiti maji Tanzania kwa ajili ya kuwafahamisha watanzania katika fursa hii muhimu na yenye faida.
Wengi katika wakulima wenzangu nchini wamekuwa wakifanya kilimo hiki kwa kufwata mkumbo na wala siyo kitaalamu, na ndiyo maana utakutana na baadhi ya watu kama siyo wengi wao wanalalamika juu ya hasara wanazopata katika kilimo hiki.

Na hii hutokana na tamaa za kupata faida haraka na kutoka kimaisha badala ya kufuata utaratibu maalumu na wakitaalamu katika kilimo ili kufikia malengo yao.

Mbegu Bora za Matikiti 

Mbegu maarufu ya tikiti ni Sukari F1, hata hivo madukani zinapatikana nyingi bora na tofauti tofauti kama vile:

  • Arashani F1 – kutoka Syngenta 
  • Apoorva F1- kutoka seminis 
  • Sukari F1 – Kutoka East Africa seeds 
  • Sugar king F1 – kutoka Africasia 
  • Juliana F1 – kutoka Kiboseed 
  • Zebra F1 – Kutoka Balton 
  • Pato F1 – Kutoka Agrichem

HALI YA HEWA
Zao hili jamii ya mbogamboga husitawi katika hali ya hewa nyuzi joto 25 hadi 30 baridi kali.
kwa upande wa mvua matikiti yanahitaji kiasi cha mvua kati ya millimita 400-600 kwa msimu. Mvua nyingi husababisha uwepo wa magonjwa ya kuvu na bakiteria ambayo huathiri mavuno.
Kwakuwa Zao la Tikiti maji halihitaji mvua nyingi hivyo hustawi vyema kipindi cha kiangazi.

UDONGO.
Zao la tikiti maji halihitaji udongo  unaotuamisha maji kuepuka magonjwa ya fangasi na wadudu waharibifu.
Zao hili linahitaji udongo wenye rutuba na Hali ya udongo kipimo cha pH iwe kati ya 6.0 na 7.0. Ingawa mmea una uwezo vile vile wa kuhimili kwenye udongo wenye pH 5.0

UKANDA UNAOFAA KWA KILIMO CHA MATIKITI MAJI TANZANIA.
Kwa upande wa Tanzania zao la tikiti maji hustawi vizuri kwenye ukanda wa pwani kama Daresalaam,Tanga, Morogoro, Mtwara, lindi na Pwani ambapo kuna hali ya hewa ya joto na jua la kutosha.

UANDAAJI WA SHAMBA
Andaa shamba kwa kulisafisha na kulitifuwa vizuri kwa tractor au jembe la mkono kisha kabla ya kusia mbegu, majani na mabaki ya shamba lililokuwa na ugonjwa yaondolewe na yateketezwe kabisa. Hii utasaidia kupunguza ueneaji wa magonjwa sumbufu katika shamba.

UPANDAJI
Panda mbegu 2 katika kila shimo lenye urefu wa 2 sentimita.
Usipande katika kitalu kwasababu miche ya mitikiti huwa ni dhaifu sana wakati wa upandikizwaji iwapo itapandwa kwenye kitalu hivyo kupelekea kufa kwa miche hiyo.

NAFASI

Sia mbegu umbali wa mita 1 kutoka shina hadi shina katika mstari na mita 2 kutoka mstari hadi mstari.

UPUNGUZAJI WA MIMEA

Mimea ya mtikiti huanza kuota, baada ya siku saba hadi wiki mbili.
Baada ya mbegu kuota punguza katika Mbegu zaidi ya moja zilizoota katika kila shimo kata mche moja na uache ule mche wenye afya zaidi ndio uendelee kukua.

KUMBUKA: katika kupunguza miche usiung’oe mche bali ukate ili kuzuia kusumbua mizizi ya mmea uliobaki. Vilevile unaweza kupandishia udongo kwenye mashina ili kusaaidia kupunguza maji kutuama kwenye mimea yako, pia unaweza kuweka samadi badala ya kupandishia udongo ukiwa na nia ileile ya kuzuia maji yasituame na kuongeza rutuba.

Kama una sehemu ndogo ya shamba unaweza kuyawekea matikiti waya ya kutambalia, ila inabidi uwe imara kwa sababu ya kuhimili uzito wa matunda.
Wakati mimea inapo anza kutambaa kwenye waya ni lazima kuielekezea kwenye waya au kamba ngumu na kuifungia.

MATANDAZO (MULCHES).
Matandazo ni nyasi, mabaki ya mimea, pumba za mpunga au malanda ya mbao ambayo hutumika kufunika ardhi ili kutunza unyevu katika udongo, kupunguza uotaji wa magugu, mimea kutambaa juu na huyazuia matunda kugusana na ardhi/udongo.
Hivyo baada ya miche kutambaaa kwa kiasi unaweza kuweka matandazo (mulches) ambayo yaweza kuwa nyasi kavu kwenye udongo ili kuzuia upotevu wa unyevu vile viile kupunguza uotaji wa magugu shambani kwako. Vile vile matandazo yakioza yanaongeza rutuba kwenye udongo na hulinda udongo dhidi ya mmomonyoko.

UWEKAJI WA MBOLEA

Weka mbolea aina ya yaramila otesha wiki moja baada ya tikiti kuota: Mbolea za viwandani aina ya NPK au mbolea zenye nitrogen mfano yaramila winner kiasi cha gram 10 hadi 20 ziwekwe wakati mimea ikianza kutambaa kwaajili ya kukuuzia.

Vilevile samadi inaweza kuwekwa wakati mimea ikiwa midogo.
 Baada ya mimea kutengeneza mauwa weka mbolea yenye potasium mfano MOP au tumia booster kama vile vegmax na mult K.
mimea ikianza kutengeneza matunda weka mbolea yenye calcium kama vile yaraliva nitrobar hadi mara 2 au 3 kwa wiki mpaka matunda yatakapokomaa.

KUMBUKA: Baada ya mmea kutoa matunda, punguza matunda na ubakishe matunda matatu au manne katika kila shina la mmea. Hii husaidia shina kuzaa matunda makubwa (kibiashara) na yenye umbo zuri la kuvutia kwa mteja.

UMWAGILIAJI
Shamba linatakiwa limwagiliwe mara kwa mara wakati mvua zinapokosekana au wakati wa mvua chache.
Kipindi muhimu zaidi ambapo mimea hii huhitaji maji ni katika kipindi cha uotaji wa mbegu, wakati wa kutoa maua na siku takribani kumi kabla ya kuvuna. Iwapo kutakuwa na ukosefu wa maji kutasababisha kutengenezwa kwa matunda ambayo si mazuri na yenye umbo baya wakati wa utengenezaji wa matunda pia upunguaji wa ukubwa wa tunda.

KUMBUKA; usimwagilie matikiti wakati wa jioni sana au usiku kwasababu inaweza kusababisha magonjwa ya majani kutokana na unyevu kukaa muda mrefu. Vile vile usimwagilie juu ya maua wakati wa asubuhi au join kwasababu unaweza kuzuia wadudu kama nyuki ambao ni muhimu sana wakati wa uchavushaji.

MAUA NA MATUNDA
Matikiti hutoa maua dume na jike kwenye tawi moja. Kwa kawaida maua dume huwa ni madogo zadi na hutoka mapema zaidi yakifuatiwa na maua jike ambayo huwa makubwa zaidi. Maua yanaweza yasionekane au yasitokee iwapo kiasi kidogo cha maji kitamwagiliwa ,upungufu wa viritubisho kwenye udongo na hali ya hewa ya joto/baridi sana n.k


Uchavushaji hufanya na wadudu na iwapo itaonekana hakuna wadudu unaweza kuchavusha kwa kutumia mkono.
Hii hufanywa kwa , kukata maua dume kwa kisu na kufanya uchavushaji kwenye maua jike, maua jike ya mwanzo kwenye tawi ndiyo yenye ukuaji bora zaidi, unaweza kukata tawi lisiendelee kukua baada ya matunda kutokeza hii husababisha kuwa na matunda makubwa zaidi. Hii inawezwa kufanywa zaidi wakati wa Asubuhi.
KILIMO CHENYE FAIDA CHA KITUNGUU MAJI 
WADUDU NA MAGONJWA YA MATIKITI
Wadudu wa matikiti wako wa aina mbalimbali na wanaoshambulia sehemu za majani na maua, na wengine hushambulia matunda, pia kuna magonjwa ya fangasi ambayo hushambulia mimea.

Magonjwa kama ukungu wa unga (powdery mildew) na wa chini (Downy mildew) na mengine yadhibitiwe kabla hayajaleta madhara kwenye mimea. Ili kujua dawa za magonjwa ni vizuri kuchukua sampuli na kwenda nayo kwenye duka la dawa na pembejeo za kilimo ili kupata dawa sahihi. Dawa aina ya Mancozeb inaweza kutumiwa kuthibiti magonjwa hayo hapo juu.

Vilevile matikiti hushambuliwa na wadudu ambao hukaa katika majani, maua na matunda. Dawa aina ya KARATE itasaidia kuua wadudu wa majani, maua na matunda.

UVUNAJI NA UHIFADHI WA MATIKITI

Kwa kawaida tikiki maji huwa tayari kwa kuvuna baada ya siku 80 hadi 100 baada ya kupanda.
Vuna wakati tunda limeiva kabisa kwa kukata kikonyo mahala kinapoanzia katika tawi kama ilivyo pichani.
Epuka kulijeruhi tunda kwa kukata kikonyo kinaposhikilia tunda.
Hifadhi katika eneo lenye ubaridi nyuzi 15 hadi 20 C. Hifadhi vizuri mahala pakavu pasipo na joto kali.

KUJUWA FAIDA.
faida hufahamika mara baada ya kujuwa mapato na gharama za uzalishaji zilizotumika.

MAPATO
Ekari moja yenye ukubwa wa 70 × 70 mita  inachukuwa miche 2450 kwa nafasi ya mita 1 kwa 2 ya mitikiti shambani.

Ukipunguza matunda katika kila shina ukabaki na matunda manne manne, utapata matunda ya matikiti maji 9,800/= kwa ekari.

Katika maeneo mengi ya Tanzania bei ya tikiti maji lenye sifa nzuri ni shilingi 2,000/= hadi 3,000/=

Mkulima akiuza matikiti kwa bei ya 2,000/= kwa tunda mkulima atapata kiasi cha 19,600,000/= (milioni kumi na tisa na laki sita)kwa ekari moja.

Endapo mkulima atauza kwa bei ya 1,000/= kwa tunda, bhasi mkulima atapata kiasi cha 9,800,000/= (million tisa na laki nane kwa ekari)

Gharama hii itaenda juu zaidi ama itapungua kutegemea na idadi ya matunda uliyoyapata katika ekari mmoja na bei ya muuzaji. Hivyo unaweza ukapata faida kubwa zaidi ukiongeza uangalizi wa shamba lako na kufuata utaratibu katika ulimaji wa zao hili.

GHARAMA
Tikiti maji linahitaji mbolea, maji, kemikali za kuua wadudu na magonjwa pamoja na maandalizi  ya shamba ambavyo gharama yake haizidi Tsh. 500,000/= katika uangalizi mkubwa

KUMBUKA: Gharama jumuishi katika hiyo 500,000/= ni za mbolea na madawa pekee.
Kwasababu gharama za mashamba na wafanyakazi hutofautiana kulingana na eneo husika 

USHAURI WA MWANDISHI. Ni vyema mkulima kujuwa Soko la mazao yake au kutafuta soko kwa kuweka mkataba na makampuni au wanunuaji wakubwa kabla hajaanza mradi wa uzalishaji, siyo kwa tikiti maji tu bali na kwa mazao mengine ya matunda na mboga mboga.

WASILIANA NAMI

+255 757 139 423 Mr Mpinga

Maoni

  1. Ahsante mkuu nimeipenda hiyo inenifungua upeo.

    JibuFuta
  2. Asante sana bro kwa elimu yako bora

    JibuFuta
  3. Elimu yako nzuri sana, ahsante kwa elimu hiyo

    JibuFuta
  4. Asante mtaalamu. Maelezo yako Nimeyapendaje Na nitazingatia. Karibu shambani

    JibuFuta
  5. kwa watakaojaribu kilimo hiki vipi unaweza kuwafanyia connection ya soko?

    JibuFuta
  6. Soko ndiyo cha muhimu zaidi

    JibuFuta
  7. Dah Yani mambo ni dire sana

    JibuFuta
  8. asante sana nimeelewa vizuri sana.

    JibuFuta
  9. Mzee nimeupenda ufahamishaji wako ni mzri sana na wa kueleweka kabisaa ,nitajitahid kufuata maelezo yako ili nifanikiwe asante sana

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Machapisho Maarufu